Dodoma/Dar. Wakati makada wanaotangaza nia na
kuchukua fomu kugombea urais kupitia CCM wakiendelea kujinadi kwa kutaja
sifa mbalimbali za rais ajaye, chama hicho kimesema hayo yote ni kazi
bure kwa kuwa chenyewe kina vigezo vyake 13 ambavyo kitavitumia kumpata
mgombea wake wa nafasi hiyo.
Makamu Mwenyekiti wa chama hicho, Philip Mangula
alisema hayo alipozungumza na waandishi wa habari mjini hapa jana huku
wasomi na wachambuzi wa siasa wakisema sifa hizo na ahadi wanazotoa
wagombea hao si rahisi kutekelezeka ndani ya mfumo uliopo wa chama
hicho.
Mangula, ambaye pia ni mwenyekiti wa kamati ndogo
wa maadili, alisema: “Kila mtu anatoa sifa zake anazozipenda. Ohh nataka
mgombea ajaye awe hivi… lakini chama chetu kimetaja sifa 13 za mgombea
urais. Mtu anayetaka kuwa mgombea kupitia CCM lazima awe na vigezo
hivyo.
Mangula alisema kifungu cha tano cha kanuni za
uteuzi wa wagombea wa CCM, kinaipa jukumu Halmashauri Kuu ya Taifa ya
chama hicho (NEC) kuzingatia mambo kadhaa muhimu wakati wa uteuzi wa
mgombea katika nafasi ya urais.
Aliyataja baadhi ya mambo hayo kuwa ni uzito wa
nafasi hiyo, haja ya kulinda na kuendeleza mshikamano miongoni mwa
wanaCCM, haja ya kupanua demokrasia ya ndani katika kuwapata wagombea na
hali halisi ya nyendo za ushindani wa kisiasa nchini.
Vigezo 13 vya urais
Mangula alitaja vigezo vya mgombea urais CCM kuwa
ni uwezo mkubwa wa kuongoza nchi kwa kutumia uzoefu katika uongozi wa
Serikali, umma au taasisi, awe mwadilifu, mwenye hekima na busara.
“Unapimaje hekima?” aliuliza Mangula na kujibu
mwenyewe: “Unapima kwa kuangalia yale mliyokubaliana kama ameyatekeleza
kama mlivyokubaliana.”
Alivitaja vigezo vingine kuwa ni elimu ya chuo
kikuu au inayolingana na hiyo, upeo mkubwa wa kudumisha na kuendeleza
Muungano, umoja, utulivu na mshikamano wa kitaifa, wepesi wa kuona
mbali, asiyeyumbishwa na mwenye uwezo wa kuona mbali kuhusu masuala
nyeti na muhimu kwa Taifa kwa wakati unaofaa.
Vigezo vingine ni upeo mkubwa na usiotiliwa shaka
kuhusu masuala ya kimataifa ili aweze kuwa kiungo imara kati ya nchi na
dunia yote, asiwe mwenye hulka ya udikteta au ufashisti, bali awe mtu
mwenye kulinda Katiba, utawala bora, kanuni na taratibu za nchi.
Mangula alisema mgombea urais wa CCM anapaswa kuwa
mtetezi wa wanyonge wa haki za binadamu na mzingatiaji wa maendeleo ya
watu wote. Pia asiwe na tamaa ya kujitafutia umaarufu wa mtu binafsi.
Pia mgombea lazima awe mstari wa mbele katika kuzifahamu, kuzieleza,
kuzitetea na kuzitekeleza sera na ilani ya uchaguzi ya CCM, awe mpenda
haki na jasiri wa kupambana na dhuluma na uonevu.
Alisema anatakiwa asiwe mtu anayetumia nafasi yake
ya uongozi kujilimbikizia mali, awe ni mtu anayekubalika na wananchi,
makini katika kuzingatia masuala ya uwajibikaji wa viongozi na
asiyevumilia uzembe wa majukumu au wajibu aliokabidhiwa ili kuinua
nidhamu ya kazi tija na ufanisi.
Post a Comment